Wednesday, May 21, 2014

Kwa Staili Hii Diamond Badilika Kabla Mambo Hayajaharibika..Kwa Mengine Hongera.

Mwaka 2014 umekuwa ni mwaka wenye neema nyingi kwa Diamond Platnumz kimataifa. Tangu aachie video ya remix ya My Number One aliomshrikisha Davido, jina la staa huyo limekuwa kubwa kiasi cha sasa kumfanya afike sehemu ambayo hakuna msanii wa Tanzania aliyewahi kufika.

Kuanzia video yake kushika namba moja kwenye vitu vikubwa vya TV kikiwemo Trace TV, kutajwa kuwania tuzo za MTV MAMA katika vipengele viwili na pia kutajwa kuwania tuzo za BET kwenye kipengele cha Best International Act: Africa. “An international music superstar from Tanzania is being born right before our eyes. Hongera sana @diamondplatnumz,” alitweet January Makamba.

Ni kweli, supastaa wa kimataifa kutoka Tanzania amezaliwa mbele ya macho yetu na ni wajibu wetu kumuunga mkono katika kila hatua anayoenda. Lakini kama unamtakia mtu heri na mafanikio zaidi, si lazima kumsifia muda wote. Ni vyema kumwambia ukweli pale ambapo tunahisi anatakiwa kuparekebisha ili asonge mbele zaidi.

Jambo muhimu ambalo Diamond anatakiwa kurekebisha ni katika live performance. Naomba nikiri kuwa pamoja na kuwa shabiki mzuri wa nyimbo nyingi za Diamond, sijawahi kupenda performance zake za live. Nimeshamhudia kwa zaidi ya mara 10 akitumbuiza na zote nimekuwa nikimuona akifanya vilevile na sipati kile ambacho nakuwa nakitegemea.

Juzi alikuwa mmoja wa wasanii waliotumbuiza kwenye show ya Road to MAMA ya MTV Base iliyofanyika Club Bilicanas akiwa pamoja na Sauti Sol na kundi la Mi Casa Music. Bahati mbaya ama nzuri kwake ni kwamba kutokana na kuwa msanii mwenyeji, yeye alikuwa msanii wa mwisho kutumbuiza. Walianza Wakenya Sauti Sol ambao kwa mtu aliyekuwa pale ukumbini atakubali kuwa show yao ilishangiliwa sana

Baadaye walifuata Mi Casa Music na wao wakadhihirisha kwanini ni kundi bora la muziki wa house kwa sasa nchini Afrika Kusini kwa kupiga show kali sana.

Diamond alifuata na kama kawaida wakati anaingia alishangiliwa mno. Kama kawaida yake, aliungana na dancers wake wanne waliokuwa wakimpa support. Ilikuwa show ya kawaida iliyoboa kwa muda mfupi tu.

Ushauri wangu kwa Diamond ni kuwa asiconcentrate sana katika kucheza na kusahau kujiimarisha katika uimbaji wa live. Haoneshi ujuzi wowote wa kuziimba nyimbo zake kiustadi anapokuwa stejini. Kwakuwa hujikuta akicheza mno na hivyo kuchoka haraka, sauti yake huharibika na kusikika vibaya na huondoa kabisa ule uprofesheno wa sauti ya msanii anayependwa na mwenye hits nyingi. Kama angekuwa anaimba na vyombo live show ingekuwa inapewa jeki na muziki tofauti unaopigwa na bendi.

Atafute namna nyingine ya kiubinifu zaidi ya uimbaji wa nyimbo zake live. Asitumbuize nyimbo kama zinavyosikika kwenye CD. Kama ataendelea na performance za kutumia DJ na CD, basi atengeneze version tofauti za beats atakazotumia kuimba live. Madhara ya hiki anachokifanya sasa ataonekana kama dancer badala ya kuwa muimbaji, sifa aliyonayo Cabo Snoop.

Kelele na shangwe anazozipata akiwa anatumbuiza zisimdanganye kuwa anazikonga nyoyo za mashabiki kwa performance kali kwakuwa ukweli ni kwamba shangwe nyingi ni kwasababu nyimbo anazoimba ni hits na wengi wanazifahamu. Kwa perfomance ya aina ile kama angekuwa ni msanii asiye na jina, wengi wasingekuwa wanarespond hivyo.

Shabiki hapendi kwenda kumuona msanii ambaye nyimbo zake hutumbuiza nyimbo zake vilevile kama zinavyosikika redioni. Kwa walioshuhudia show ya P-Square November mwaka jana pale Leaders Club waliona jinsi mapacha hao walivyo wachawi wa live performance.

Pamoja na kuwa wachezaji wazuri, hawakuwa wakicheza katika kila wimbo. Muda mwingi walikuwa wakiimba nyimbo zao kwa hisia na kuinteract vizuri na watazamaji.

Kwakuwa kutajwa kwake kwenye tuzo hizo kubwa kutampa exposure zaidi na kupata show za kimataifa, alifanyie kazi hilo ili kutowapa sababu wakosoaji na kumuona kama amebebwa tu kufika hapo.
Bongo5

No comments:

Speak Your Mind

Powered By Blogger · Designed By Seo Blogger Templates